Zaburi 75
Mungu Ni Mwamuzi 
Kwa mwimbishaji. Mtindo wa “Usiharibu!” Zaburi ya Asafu. Wimbo. 
 1 Ee Mungu, tunakushukuru, 
tunakushukuru wewe, 
kwa kuwa jina lako li karibu; 
watu husimulia matendo yako ya ajabu. 
 2 Unasema, “Ninachagua wakati maalum; 
ni mimi nihukumuye kwa haki. 
 3 Wakati dunia na watu wake wote inapotetemeka, 
ni mimi ninayezishikilia nguzo zake imara. 
 4 Kwa wale wenye majivuno ninasema, 
‘Msijisifu tena,’ 
kwa wale waovu, ‘Msiinue pembe zenu. 
 5 Msiinue pembe zenu dhidi ya mbingu; 
msiseme kwa shingo zilizonyooshwa.’ ” 
 6 Hakuna yeyote atokaye mashariki wala magharibi 
au kutoka jangwani awezaye kumkweza mwanadamu. 
 7 Bali Mungu ndiye ahukumuye: 
Humshusha huyu na kumkweza mwingine. 
 8 Mkononi mwa Bwana kuna kikombe 
kilichojaa mvinyo unaotoka povu 
uliochanganywa na vikolezo; 
huumimina, nao waovu wote wa dunia 
hunywa mpaka tone la mwisho. 
 9 Bali mimi, nitatangaza hili milele; 
nitaimba sifa kwa Mungu wa Yakobo. 
 10 Nitazikatilia mbali pembe za waovu wote, 
bali pembe za wenye haki zitainuliwa juu.